Ijumaa, 31 Januari 2025

KUWA IMARA

 

Kijana mmoja aliyekuwa anacheza mpira na alikuwa ana ndoto kubwa kutoka kuwa mchezaji wa kitongoji mpaka kuwa wa kimataifa, lakini katika ndoto hiyo alipitia changamoto nyingi kuanzia kwa mwalimu wake na hata wenzake walikuwa wanamvunja moyo mpaka yeye binafsi kuanza kuona kuwa ndoto yake inashindwa kutimia , lakini siku moja majira ya jioni alikuwa anarudi nyumbani baada ya kutoka katika mazoezi ya mpira, akiwa amechoka sana pamoja na kutingwa na mawazo mengi yaliyokosa mwanga na huku moyo wake ulikuwa una dunda kama gari lililokosa mwelekeo na kuanza kuelekea kwenye maporomoko makali………akiwa katika hali hiyo ya giza ghafla akatokea mzee mmoja aliyekuwa akiishi jirani naye na kumwambia neno hili “ kijana uwe imara utashinda “ hilo neno liliingia mifupani, kwenye damu na nyama na hatimaye kufuta giza lililokuwa likitawala kichwa chake! Ni kama kipofu kuona mwanga kwa mara ya kwanza.

Hivyo yule kijana akaanza kutembea katika neno la yule mzee kuliko maneno ya watu wengine waalimu na wachezaji wenzake waliokuwa wakimvunja moyo na hatimaye katika bidii yake siku moja alitimiza ndoto yake na kwenda kucheza katika mataifa mengine sawa na ndoto yake.

- kuna vitu viwili katika maisha ya mtu kuna NDOTO na TAMAA YA MTU BINAFSI, mara nyingi tamaa inaweza isitimie.

Karibu!

Ni muhimu ujue uimara unajengwa ndani ya mtu husika katika kuyakabili mambo yaliyo kinyume naye au yanayo mzunguka.

Unahitaji uimara wa ndani ili kushinda mazingira yote.

- usikubaliane na mazingira vile yanavyosema maana Mungu yuko nje ya mazingira.

2 Wafalme 7:1 Elisha akasema, Lisikieni neno la Bwana; Bwana asema hivi, Kesho panapo saa hii, kipimo cha unga mzuri kitauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, langoni pa Samaria.

 2 Basi yule akida, ambaye mfalme alikuwa akitegemea mkono wake, akamjibu yule mtu wa Mungu, akasema, Tazama, kama Bwana angefanya madirisha mbinguni, je! Jambo hili lingewezekana? Akamwambia, Angalia, wewe utaliona kwa macho yako, lakini hutakula.

 

Ni matamanio ya wengi kuwa katika mazingira yaliyo kuwa shwari maana hapo hisia na vionjo vya mwili hutulia, Lakini sio wakati wote unaweza kuwa na mazingira uyapendayo kuna wakati bahari inachafuka lakini utahitaji kuvuka.

Ndomana hata katika vyombo vya habari pindi bahari inapochafuka huwa wanashauri safari za majini zisitishwe kwa muda mpaka pale hali ya hewa itakapo kuwa shwari.

Kuna wakati mambo yanachafuka/ yanakuwa visivyo au nje ya matarajio yako ama mpangilio kuharibika ili kitu KIPYA KIZALIWE maana kuna vitu vingine haviwezi kudhihirika katika mazingira ya kawaida.

Kuna baadhi ya machafuko/ kutoelewana na mtu wako wa karibu kunatokea sio kwamba mmechokana la hasha! Bali kuna kitu kinazaliwa hapo kitakacho kupeleka wewe katika kuyafurahia maisha yako zaidi lakini pindi usipoelewa unaweza kujikuta katika wimbi la chuki na kisasi kisichokuwa cha lazima.

Kuna mambo mengine ili yatokee kwanza yanakutenganisha na yale mambo uliyo yazoea au unayo yapenda.

² Lutu na Abramu

 Mwanzo 13:5 Na Lutu aliyesafiri pamoja na Abramu, yeye naye alikuwa na makundi ya ng'ombe na kondoo, na hema.

 6 Na ile nchi haikuwatosha, ili wakae pamoja; maana mali zao zilikuwa nyingi, hata wasiweze kukaa pamoja.

 7 Kukawako ugomvi kati ya wachunga wanyama wa Abramu, na wachunga wanyama wa Lutu; na siku zile Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi.

 8 Abramu akamwambia Lutu, Basi, usiwepo ugomvi, nakusihi, kati ya mimi na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu ndugu.

 9 Je! Nchi hii yote haiko mbele yako? Basi ujitenge nami, nakusihi; ukienda upande wa kushoto, nitakwenda upande wa kuume; ukienda upande wa kuume, nitakwenda upande wa kushoto.

 10 Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla Bwana hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya Bwana, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari.

 11 Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao.

 

 

Unahitaji kuyakubali mazingira mageni pasipo manung’uniko ili maisha mapya yazaliwe.

Natambua mahali panapokuwa katika machafuko unakuwa kama uko gizani pasipo matumaini ya mwanga unaweza usijue lini utaona mwanga.

² hakuna jaribu lisilo na mlango

1 wakorintho 10:13 Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.

 

Unahitaji ujasiri tu ili uweze kuruhusu nguvu ya kupindua giza kuwa nuru lasivyo unaweza kujikuta maisha yako yote umeatamia giza.

Yohana 1:5 Nayo nuru yang'aa gizani, wala giza halikuiweza.

 

INAITWA SIKU! BARIKIWA SANA

 

Imeandaliwa na:

Cothey  Nelson………………………………………………………………………………0764 018535

Ijumaa, 17 Januari 2025

KAA KATIKA KITI CHAKO.

 


Moja ya kitu kizuri ni kukaa sehemu uliyoandaliwa kukaa, na sio sehemu unayoitaka wewe kukaa.

Unapokaa sehemu unayopaswa kukaa bila shaka kuna faida nyingi zitaelekezwa hapo kwa kutambua sehemu hiyo imekaliwa na mtu husika.

Wakati mwingine unaweza kutamani kukaa katika kiti ambacho sio chako / haujaandaliwa wewe japo kinaweza kuwa katika eneo zuri ambalo watu wengi wakiangalia hapo wangekuona wewe basi nawe ungejisikia vizuri.

Unapokaa mahali au sehemu sio yako ama hujapangiwa bila shaka unaweza kupata mambo usiyotarajia kwa kuwa umekaa sehemu isiyo yako baada ya kupafurahia ukakuta unaboreka.

Mathalani unapokaa sehemu sio yako unaweza kukuta wewe ni mnywaji wa soda unaweza kuletewa bia, unaweza kuona wamekudharau au wamekuonaje?

Pia katika hali ya kawaida unaweza kujikuta umechoka kukaa katika sehemu moja kwa muda mrefu hali ya hewa inaweza kubadilika mathalani kuna wakati inaweza kuwa mvua au jua ukatamani kuhamia upande mwingine unaweza kujikuta umeshindwa kurudi upande ulipokuwa umekaa hapo awali.

Kila mahali  pana ukaaji wake msibani au harusini  huwa kuna utaratibu wake kila sehemu kuna wahusika wake mathalani huwezi kuingia katika harusi alafu ukakaa mahali bibi harusi anakaa na we ukatulia tuli na kuanza kuperuzi mtandaoni kwenye simu yako na amani tele na hata watu wakiingia wewe bado umekaa tu utafikiri mpambaji.

Ni muhimu utamani na ufurahie kukaa katika kiti chako/ sehemu yako.

Kwasababu kuna baadhi ya mambo unaweza kuyakosa kwa kukosa kukaa sehemu uliyopaswa kukaa.

Yakupasa kujua kuwa sehemu yako tu, ndio iliyobeba ustawi wako na Mungu anakusudi kamili la wewe kukuweka hapo haijalishi hayo mazingira yanaonekanaje au yanatoa mtazamo gani kwa mtu au kwa watu.

Unapaswa kujua Mungu anapokuweka hapo ana kuandaa kwa ajili ya utukufu wake maana wewe umetokana na yeye.

Ni muhimu utambue sehemu yako ni ipi popote ulipo ili ufanye kwa ufanisi mkubwa maana unaweza kujikuta unatembea katika maeneo ya wengine na kuwasaidia huku sehemu yako ikibaki kama ilivyo pasipo kufanyiwa kazi yoyote.

Pia ni vizuri utambue kuwa sisi kama mwili katika kristo ni viungo kila mmoja kwa mwenzake, katika mwili wa binadamu kazi ya jicho haiwezi kufanywa na mkono hivyo tambua unaposimama kama jicho basi hapo unakuwa mwanga na usaidizi katika mkono katika kuendelea na majukumu yake pia unaleta ladha na mng’ao wa tofauti na tija katika mwili wote, maana viungo katika mwili wa binadamu vinahitajiana ili mwili uweze kufanya kazi yake katika hali ya ubora.

Ni lazima utamani kukaa katika kiti chako ili uweze kupata mema ya mbingu na sio mema ya dunia kwa kitambo.

Bila shaka unapofurahia kiti chako na kukaa kwa kutulia mbele za Mungu utapelekea watu waone ukuu wa Mungu kupitia wewe.

 

INAITWA SIKU! BARIKIWA SANA

Imeandaliwa na:

Cothey  Nelson………………………………………………………………………0764 018535

Ijumaa, 3 Januari 2025

HATMA YAKO IMEFICHWA NDANI YA MUNGU

 



NENO “ FICHA “ limebeba usiri mwingi sana.

Limejikita katika hali ya ubinafsi zaidi!

Naam Pindi unapo tambua mahali ambapo umeficha hazina yako iko salama na hakuna mtu anaweza kuiona wala kuichukua bila shaka unakuwa na raha isiyo ya kifani ndani na nje yako.

 Mathayo 6:19 Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba;

 20 bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi;

 

*     *     *      *       *        *       *           *          *          *           *           *         *          *         *

Maadamu umezaliwa tu basi ujue hatma yako iko ndani ndomana ukapelekea wewe kuzaliwa.

Hatma wakati mwingine uitwa KUSUDI LA WEWE KUWEPO, hivyo maadamu umezaliwa unasababu ya kuzaliwa la sivyo usingezaliwa! Kama taasisi inapohitaji kuongeza mfanyakazi bila shaka kuna kuwa na wajibu pamoja na haki ya mfanya kazi aliyekuwepo na atakayeingia.

- uhitaji wa hiyo taasisi ndio unapelekea sababu ya kuajiri.

Hivyo duniani pasingekuwa na uhitaji wako, Mungu asingeruhusu wewe uzaliwe, hivyo kila mtu ili mradi amezaliwa pasipo kuangalia amezaliwaje basi liko kusudi la kuzaliwa kwake.

Kusudi/ hatma sio swala au jambo la kumuomba Mungu akupe ila kinacho hitajika hapo ni udhihirisho tu maana tayari Mungu amekiungamanisha na maisha yako.

Hivyo sio rahisi mtu kukutenganisha na hatma yako, maana ni Mungu amekiweka kwa kusudi maalum ( special mission ) na hakuna mwanadamu yeyote atayeweza kukiondoa au kukichukua.

Japo, Ni kweli unaweza kuwa na hatma kubwa lakini unaweza kushindwa kudhihirika au kufanyia kazi hivyo ukawa hasara baada ya kuwa faida.

 

 

 

² Mwenye talanta moja

Mathayo 25:24 Akaja na yule aliyepokea talanta moja, akasema, Bwana, nalitambua ya kuwa wewe u mtu mgumu, wavuna usipopanda, wakusanya usipotawanya;

 25 basi nikaogopa, nikaenda nikaificha talanta yako katika ardhi; tazama, unayo iliyo yako.

 26 Bwana wake akajibu, akamwambia, Wewe mtumwa mbaya na mlegevu, ulijua ya kuwa navuna nisipopanda, nakusanya nisipotawanya;

 27 basi, ilikupasa kuiweka fedha yangu kwa watoao riba; nami nikija ningalipata iliyo yangu na faida yake.

 28 Basi, mnyang'anyeni talanta hiyo, mpeni yule aliye nazo talanta kumi.

 

² mti usiozaa uvumilia

Luka 13:7 Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu; uukate, mbona hata nchi unaiharibu?

 8 Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi;

 9 nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate.

 

Mungu anahuzunika pindi anapoiweka hatma kubwa ndani yako anapoona hauitumii na wakati mwingine hata hauitambui kama unayo hatma ndani yako.

 Hosea 4:6 Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako.

 

Mungu anapoweka hatma ndani yako ina maana amekupa ufunguo wa mafanikio yako.

- unaposhindwa kulitumikia kusudi lako basi unajichelewesha katika mafanikio yako.

Maana unapofanya jambo lililoshikamana na hatma yako inakuwa ni sawasawa na maji yanayotoka kwenye kisima kisicho kauka.

Vitu muhimu katika hatma yako ni kuitambua hatma yako iliyo ndani na kujua wakati sahihi wa kuitumikia hiyo hatma na kuhakikisha unaitumikia katika viwango vya hali ya juu.

 

Mng’ao wako uko pale utakapoanza kulitumikia kusudi au hatma.

- unapoipenda hatma yako ina maana maana umejipenda wewe.

Kwa lugha nyepesi tunaozungumzia hatma tunazungumzia kazi za Mungu alizoziweka ndani yakoili uweze kufanya badala yake.

Waefeso 2:10 Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo.

Yakupasa kujua haupo kuangalia dunia inavyokwenda bali unamchango katika kubadilisha dunia yako haijalishi ni dogo au kubwa.

Ni hatari sana kuishi ukitamani matokeo ya watu wanaoishi kwenye hatma zao ukafikiri Mungu amewapendelea zaidi yako.

Na wewe ukiishi katika kujitambua utapelekea wengine kuanza kukutamani na kukufanya kuwa wewe ni mfano kwao.

Ili uweze kutembea katika hatma yako katika faida ni lazima kwanza utembee katika Mungu, maana yeye ndiye anayejua kwanini amekuchagua na akaweka hiyo hatma na kwa ajili ya nini?

 

Yakupasa kujua tija yako mbele za Mungu ni pale utakapoamua kuishi kwenye hatma yako kwa msaada wa Roho mtakatifu.

 

INAITWA SIKU! BARIKIWA SANA

Imeandaliwa na:

Cothey  Nelson………………………………………………………………………..0764 018535